Klabu ya Simba imedhamiria kuionyesha Afrika uzinduzi wa
jezi mpya itakayotumiwa katika msimu wa mwaka 2023/2024 tukio hilo ambalo
litafanyika katika Kilele cha Mlima Kilimanjaro almaarufu Paa la Afrika.
Zoezi linalotegemea kufanyika Julai, 21 katika kilele cha
Mlima Kilimanjaro chenye urefu wa mita 5895 kutoka usawa wa bahari.
Akizungumza katika hafla ya kuwaaga wapanda Mlima hao
kupeleka jezi katika kilele cha Mlima Kilimanjaro Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa
Kilimanjaro, Mhe. Abdallah Mwaipaya aliipongeza Klabu ya Simba kwa ubunifu huu
na uzalendo wa kuitangaza nchi yao.
“Hili ni tukio kubwa ambalo Klabu ya Simba wamelifanya
kuuongezea thamani Mlima Kilimanjaro na utalii kwa ujumla kwa nchi yetu,
niwatake mashabiki wote wa Simba waliopo katika mikoa ya jirani na Kilimanjaro
kujitokeza kwa wingi kuwapokea wapandaji Mlima wanaporejea siku ya jumamosi”
alisema Mhe.Mwaipaya.
Naye, Msemaji wa Simba SC Ahmed Ally alisema “Jezi zetu
zitazinduliwa Julai, 21 2023 Juu ya Kilele cha Mlima Kilimanjaro saa 1:00 Usiku
tukio litakalokuwa Mubashara kutoka Mlimani” Amesisitisa Ahmed Ally.
Pia, Ahmed Ally alielezea sababu za jezi ya Simba SC
kuzinduliwa katika kilele cha mlima Kilimanjaro ni kutokana na maono ya kuiunga
mkono serikali kwenye suala zima la kutangaza na kukuza utalii wa ndani.
“Nyote mnafahamu kwa muda wa miaka mitano sasa tumekuwa
tukitumia utambulisho wa ‘VISIT TANZANIA’ katika jezi zetu na katika jezi ya
msimu uliopita ilikuwa na alama ya Mlima Kilimanjaro hii ni ishara kwamba Simba
tupo bega kwa bega na Serikali kupigania utalii wa nchi yetu” alisema Ahmed
Ally.
Vile vile, Ahmed Ally alisema kuweka nembo za mlima huo
katika jezi zetu tuliona haitoshi na kuamua ni lazima Afrika na Dunia nzima
kuona jezi hiyo na kutambulisha utalii na Mlima wetu.
Kwa upande wake, Kaimu Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Kilimanjaro
Afisa Uhifadhi Mkuu, Mapinduzi Mdesa alitoa rai kwa klabu nyingine nchini kuiga
mfano wa Klabu ya Simba nakuja na mawazo mengine ya kutangaza utalii wetu.
“Huu ni ubunifu ambao Klabu ya Simba imekuja nao kama
Hifadhi tunachukulia ni jambo zuri sana katika kutangaza utalii wa ndani hivyo
kupitia zoezi hili tunaimani kwamba inaenda kuhamasisha watanzania wengi lakini
pia waafrika na watu wote duniani kuvutiwa kupanda Mlima Kilimanjaro, nitoe
wito kwa klabu zingine kuja na ubunifu wao kupitia maeneo yaliyohifadhiwa
ikiwemo Hifadhi ya Taifa Kilimanjaro kuja kufanya hamasa kwa mashabiki wao na
kwa watanzania kwa ujumla”.
Na. Edmund Salaho- Kilimanjaro
0 Maoni