Waziri wa Mambo ya Ndani ya
Nchi, Patrobas Katambi, amewataka vijana nchini kuipenda nchi yao,
kulinda amani na kuendelea kuwa wazalendo ili kushiriki kikamilifu
katika maendeleo ya taifa.
Katambi ametoa wito huo wakati wa
uzinduzi wa Jukwaa la Vijana uliofanyika katika Chuo cha Mipango
mkoani Dodoma. Amesema Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan
imeendelea kuweka mazingira rafiki kwa vijana kupitia kuanzishwa kwa
Wizara ya Vijana, hatua inayolenga kusikiliza na kutatua changamoto
zinazowakabili pamoja na kuwawezesha kiuchumi.
“Vijana ni
nguvu kazi ya taifa, hivyo wanapaswa kuipenda nchi yao, kulinda amani
na kutumia fursa zilizopo ili kuchangia maendeleo ya Tanzania,”
amesema Katambi.
Aidha, amesema Serikali imeendelea kuweka
mikakati mbalimbali ikiwemo utoaji wa mikopo kwa vijana ili
kuwajengea uwezo wa kujiajiri na kuboresha maisha yao. Amewahimiza
vijana kuchangamkia fursa hizo kwa manufaa yao binafsi na taifa kwa
ujumla.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir
Shekimweri, ameipongeza Serikali kwa kuendelea kuwaunganisha vijana
kupitia majukwaa mbalimbali ya majadiliano na ushiriki katika
maendeleo.
“Ofisi yangu itaendelea kutumia majukwaa haya
kusikiliza maoni ya vijana na kushughulikia kero zao kwa wakati ili
kuhakikisha wanashiriki kikamilifu katika maendeleo ya jamii na
taifa,” amesema Shekimweri.
Katika kongamano hilo, vijana
walipatiwa elimu kuhusu namna ya kutoa maoni yao katika maboresho ya
dodoso la Baraza la Vijana, Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana
toleo la mwaka 2024, elimu ya uraia, uzalendo na kujitolea, pamoja na
fursa za kiuchumi zinazopatikana katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma
na nchini kwa ujumla.

0 Maoni