Tanzania yashiriki mkutano wa kimataifa wa usimamizi wa misitu ya miombo

 

Tanzania imeibuka kivutio katika Mkutano wa Tatu wa Nchi 11 zinazotekeleza Mradi wa Usimamizi Shirikishi wa Misitu ya Miombo unaoendelea mjini Maputo, Msumbiji, baada ya kuonesha mafanikio katika uhifadhi na kuendeleza ufugaji nyuki endelevu.

Mkutano huo unaoratibiwa na Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO) umeanza Septemba 29 na unatarajiwa kumalizika Oktoba 3, 2025, ukiwaumisha zaidi ya washiriki 200 kutoka mashirika ya kimataifa, kikanda na kitaifa.

Tanzania imewakilishwa na Kamishna wa Uhifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Prof. Dos Santos Silayo, akiongoza timu ya wataalamu kutoka taasisi mbalimbali.

Wengine walioungana naye ni Mratibu wa Mradi wa Miombo, Dkt. Zainabu Bungwa (TFS), pamoja na Dr. Deogratius Paulo kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, na waratibu wa miradi ya kimataifa wa GGWI na UNCCD – Bw. Malik Malik na Bw. Timotheo Mande. FAO Tanzania imeshiriki kupitia Bw. Charles Tullah, Msaidizi wa Mwakilishi Mkazi, akiambatana na Mratibu wa Programu, Bw. Jonathan Sawaya.

Katika banda la Tanzania, zilijadiliwa mada kuhusu matumizi ya mfumo wa Honey Traceability kusimamia mnyororo wa thamani wa mazao ya nyuki pamoja na nafasi ya nyuki katika kuhifadhi misitu na kuongeza kipato cha jamii. Semina ziliendeshwa na Mhifadhi Mwandamizi Linda Shio na Wawa Mohamed kutoka Chuo cha Nyuki.

Prof. Silayo alisema mafanikio yaliyowasilishwa yamechochewa na ushirikiano mpana kati ya serikali, jamii na wadau wa kimataifa, na kwamba mazao ya nyuki yananufaisha si serikali pekee bali pia wananchi wanaoshiriki katika uhifadhi.

 “Jamii imewezeshwa kupitia ufugaji nyuki na shughuli za uhifadhi, ndiyo maana banda la Tanzania limevutia mamia ya washiriki,” alisema.




Chapisha Maoni

0 Maoni