Fuoni, Chamwino na Mbagala Kuu kupiga kura Desemba 30 - INEC

 

Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) imetangaza kuwa uchaguzi mdogo wa ubunge katika Jimbo la Fuoni, Zanzibar, pamoja na chaguzi ndogo za udiwani katika kata mbili nchini, utafanyika Desemba 30, 2025.

Taarifa hiyo imetolewa leo, Oktoba 3, 2025, na kusainiwa na Mkurugenzi wa Uchaguzi wa INEC, Ramadhani Kailima, ikieleza kuwa hatua hiyo inafuatia vifo vya wagombea waliokuwa wakiwania nafasi hizo.

Kwa mujibu wa INEC, uchaguzi wa ubunge katika Jimbo la Fuoni, Wilaya ya Magharibi B, ulisitishwa Septemba 25, 2025 kufuatia kifo cha aliyekuwa mgombea wa CCM, Abass Ali Mwinyi.

Aidha, chaguzi nyingine mbili za udiwani zitafanyika katika Kata ya Chamwino, Jimbo la Morogoro Mjini, na Kata ya Mbagala Kuu, Jimbo la Mbagala, Dar es Salaam. Nazo ziliahirishwa baada ya vifo vya wagombea waliokuwa wamepangwa kushiriki.

“Siku ya kupiga kura kwa ubunge wa Jimbo la Fuoni na udiwani katika kata za Chamwino na Mbagala Kuu itakuwa Jumanne, Desemba 30, 2025,” imeeleza taarifa ya INEC.

Tume hiyo imefafanua kuwa maamuzi hayo yamezingatia masharti ya Kifungu cha 68(1), (3) na (4) pamoja na Kifungu cha 71(2) cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024.

Kwa mujibu wa INEC, ratiba mpya ya uchaguzi kwa maeneo husika tayari imetolewa, na wadau wa uchaguzi wametakiwa kufuata taratibu zilizowekwa kwa mujibu wa sheria.

Chapisha Maoni

0 Maoni