CUF yaaahidi nyumba za kisasa kwa watumishi wa umma

 

Chama cha Wananchi (CUF) kimeahidi kuwa endapo kitapewa ridhaa ya kuongoza Serikali baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu, kitahakikisha kila mtumishi wa umma nchini anajengewa nyumba ya kisasa, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuboresha maisha yao na kupambana na mizizi ya rushwa katika taasisi za umma.

Mgombea urais wa chama hicho, Gombo Samandito Gombo ametoa ahadi hiyo Septemba 5, 2025,  wakati wa mkutano wa kampeni uliofanyika katika Kata ya Malunga, Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.

“Watumishi wa umma wengi wanapitia maisha magumu, hali inayowasukuma kuomba au kupokea rushwa. Serikali ya CUF itakapoundwa, kila mtumishi atajengewa nyumba ya kisasa. Tutaondoa njaa na shida, ili watoe huduma kwa uadilifu,” alisema Gombo.

Msaada wa Kifedha kwa Wazee kuanzia Miaka 60

Katika hatua nyingine, mgombea huyo wa urais aliahidi kuwa Serikali ya CUF itakapoundwa, itatoa fedha ya kujikimu kwa kila mzee mwenye umri wa miaka 60 na kuendelea, bila kujali kama alikuwa mtumishi wa Serikali au la.

“Hata kama mzee huyu hakufanya kazi serikalini, lakini aliitumikia nchi kupitia kilimo chake, uvuvi wake au ufugaji wake. Wote hao watajumuishwa kwenye mpango wa kupata pesa ya kujikimu kila mwezi. Rasilimali tulizonazo zinatosha kwa kila Mtanzania kuishi kwa furaha,” alisema.

Chapisha Maoni

0 Maoni