Ajali ya gari na pikipiki yaua mmoja, yaacha majeruhi Shinyanga

Mtu mmoja amefariki dunia na mwingine kujeruhiwa katika ajali ya gari na pikipiki iliyotokea usiku wa kuamkia leo Septemba 26, 2025 katika eneo la Lalsela, Kata ya Samuye, Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, mkoani Shinyanga.

Ajali hiyo ilitokea majira ya saa 7:00 usiku na kuhusisha gari aina ya Toyota Kluger lililokuwa likiendeshwa na Fabian Manoga (36), mkazi wa Tabora, ambalo lilimgonga mwendesha pikipiki aina ya SUNLG, Sudi Dotto (20), ambaye alifariki dunia papo hapo.

Taarifa ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Shinyanga, imethibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kueleza kuwa pia kijana mwingine aliyefahamika kwa jina la Noel Paul (18), mkazi wa eneo hilo, alijeruhiwa na anaendelea kupatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga.

“Ajali hiyo ilisababishwa na uzembe wa dereva wa gari ambaye alikuwa akiendesha kwa mwendo kasi na kuvuka upande usio sahihi wa barabara, kisha kugonga pikipiki iliyokuwa mbele yake,” alisema Kamanda huyo.

Kwa mujibu wa Kamanda huyo, mwili wa marehemu umehifadhiwa katika Hospitali ya Manispaa ya Shinyanga, ukisubiri taratibu za mazishi.

Aidha, Jeshi la Polisi limeendelea kutoa wito kwa madereva na watumiaji wengine wa barabara kuchukua tahadhari na kuzingatia sheria za usalama barabarani ili kuepusha ajali.

“Tunawakumbusha madereva wote kuwa waangalifu, kufuata alama na sheria za usalama barabarani wakati wote wanapotumia vyombo vya moto. Usalama wa maisha ya watu uko mikononi mwao,” alisisitiza Kamanda huyo.

Ajali hiyo imeacha simanzi kubwa kwa wakazi wa eneo la Lalsela, huku familia ya marehemu ikieleza kupokea kwa huzuni taarifa za kifo cha kijana wao ambaye alikuwa bado anajiandaa na maisha ya kujitegemea.


Chapisha Maoni

0 Maoni