Dkt. Mpango ahimiza uandishi wa habari za taswira nzuri ya Afrika

 

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango amesema wakati umefika kwa wanahabari wa Kiafrika kuonesha taswira nzuri ya Bara la Afrika kwa kuandika habari chanya zenye nguvu na za kutia moyo kuhusu Bara hili.

Makamu wa Rais amesema hayo wakati akifungua Mkutano wa Mabaraza Huru ya Habari Afrika unaofanyika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC). Amesema kwa kipindi kirefu Bara la Afrika limekuwa likitegemea simulizi za vyombo vya habari vya nje ambazo zimejikita katika hatari, vita, migogoro, na kushindwa huku vikipuuza uwezo mkubwa, uthabiti, na maendeleo ya watu wa Afrika.

Amesisitiza umuhimu wa kuwa na habari zinazoonyesha ushindi wa jamii za Kiafrika, wajasiriamali wa biashara maarufu duniani, ubora wa kitaaluma wa wanafunzi wa Afrika, uvumbuzi wa vijana, ujasiri wa wanawake na michango inayoongezeka ya Afrika katika sayansi, teknolojia, utawala bora, na uchumi wa kimataifa.

Makamu wa Rais amesema ni vema kuanza kuandika historia ya Bara hili kwa maneno na sauti ya Wafrika wenyewe. Amesema Katika kuendeleza Ajenda ya 2063 ya Umoja wa Afrika, ambayo inatazamia kuwa na bara lenye amani, umoja, ustawi na heshima ya kimataifa, vyombo vya habari lazima vichukue jukumu la kuleta mabadiliko. Amesema ni lazima kutumika kama daraja linalounganisha mataifa, kuwezesha mazungumzo yenye maana katika Bara zima na kulinda utajiri wa urithi wa kihistoria na kitamaduni wa Afrika kwa vizazi vijavyo.

Pia Makamu wa Rais ametoa wito kwa washiriki wa Mkutano wa Kimataifa wa Mabaraza Huru ya Habari kuandaa mapendekezo ikiwemo ya kisheria au maeneo ambayo yanahitaji kuboreshwa ili kutumia vyema manufaa ya Akili Unde (AI) katika tasnia ya habari.


Chapisha Maoni

0 Maoni