EU kutoa bilioni 40.8 uhifadhi bahari na usawa Zanzibar

 

Umoja wa Ulaya (EU) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wamesaini makubaliano mawili muhimu yanayolenga kukuza maendeleo endelevu, uhifadhi wa bahari, na usawa wa kijinsia.

Makubaliano hayo yalisainiwa mbele ya Mhe. Riziki Pembe Juma, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto; Rita Laranjinha, Mkurugenzi Mtendaji wa Masuala ya Afrika wa Huduma za Nje za Umoja wa Ulaya; na Hans Stausboll, Kaimu Mkurugenzi wa Kamisheni ya Umoja wa Ulaya Kanda ya Afrika, pamoja na maafisa waandamizi wa serikali na wadau wa maendeleo.

Makubaliano ya kwanza, yenye thamani ya TZS bilioni 32 (€ milioni 11), yanahusu uhifadhi wa bahari kupitia Mradi wa Bahari Yetu. Mradi huu, unaotekelezwa na Shirika la Kimataifa la Uhifadhi wa Mazingira (IUCN), unalenga kushughulikia changamoto muhimu za kulinda rasilimali za bahari, kukuza uvuvi endelevu, na kupambana na uchafuzi wa plastiki. Aidha, mradi huu utaziwezesha jamii za Zanzibar kiuchumi kwa kuanzisha fursa za maendeleo endelevu huku ukihifadhi bioanuwai tajiri ya bahari ya Zanzibar.

Makubaliano ya pili yanatenga TZS bilioni 8.8 (€ milioni 3) kupitia mpango wa Umoja wa Ulaya wa Gender Transformative Action Zanzibar, unaotekelezwa na UN Women kwa kushirikiana na wizara inayohusika na masuala ya jinsia Zanzibar. Mpango huu unalenga kuondoa vikwazo dhidi ya haki za wanawake na kuimarisha nafasi za uongozi wa wanawake katika sekta za umma na binafsi. Aidha, mkazo mpya utawekwa kwenye kukuza elimu ya wasichana, hususan elimu ya juu.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Bi. Laranjinha alisema: “Makubaliano haya yanaonyesha dhamira ya Umoja wa Ulaya katika kuleta maendeleo Zanzibar, hususan katika sekta za uchumi wa buluu na kuimarisha usawa wa kijinsia na uwezeshaji wa wanawake.”

Kwa upande wake, Bw. Stausboll aliongeza: “Makubaliano haya ni ushuhuda wa dhamira ya Umoja wa Ulaya ya kuleta manufaa na maendeleo ya kudumu kisiwani Zanzibar. Miradi hii italeta ustawi wa pamoja,, na ujumuishaji wa kijamii.”

Awali, Laranjinha na Stausboll walifanya mazungumzo na Rais wa Zanzibar, Dk. Hussein Mwinyi, kabla ya kushiriki hafla ya utiaji saini. Mnamo tarehe 10 Desemba, wanatarajiwa kushiriki katika Mazungumzo ya Ushirikiano kati ya Umoja wa Ulaya na Serikali ya Tanzania, hatua inayotegemea kuimarisha ushirikiano wa muda mrefu na kushughulikia vipaumbele vya pamoja vya pande zote mbili.



Chapisha Maoni

0 Maoni