Kipindi cha Mastaa wa China cha “Divas Hit the Road” kurekodiwa Tanzania

 

Mastaa kutoka China wakiwemo nguli wa televisheni, filamu na muziki wametua leo jijini Arusha kuelekea Hifadhi ya Taifa ya Serengeti na maeneo mengine ya nchi kurekodi moja ya vipindi vinavyotazamwa zaidi nchini humo cha televisheni kiitwacho “Divas Hit the Road.”

Katika kipindi hicho, mastaa hao hutakiwa,  kama ilivyokuwa kwenye mtindo wa filamu ya “Royal Tour” aliyoshiriki Mhe Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuishi maisha ya kawaida wakiwa bila ya walinzi wala wasaidizi wao wakitembelea nchi mbalimbali duniani ambapo kwa Afrika Tanzania itakuwa nchi ya tatu baada ya Afrika Kusini na Namibia.

Akiwapokea wageni hao kwenye Uwanja wa Ndege wa Arusha leo Jumamosi Agosti 10, 2024, wakitokea Zanzibar walikoanzia kurekodi kipindi hicho, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi, amesema ujio wa mastaa hao utasaidia mkakati wa kuitangaza zaidi nchi yetu katika soko la utalii, biashara na uwekezaji nchini China na duniani kwa ujumla.

“Kama mnavyojua mwaka huu Mhe. Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan alianzisha mkakati wa kujitangaza China kwa kurekodi filamu maalum kwa soko la nchi hiyo iitwayo “Meilii Tansaniya” (Amazing Tanzania) pamoja na staa wa filamu wa China Jin Dong. Ujio wa madiva hawa leo ni mwendelezo wa mkakati huo,” alisema Dkt. Abbasi na kuongeza kuwa Waziri wa Utalii, Mhe. Angellah Kairuki, pia atashiriki kwenye kipindi hicho Agosti 12 mwaka huu.

Kipindi cha “Divas Hit the Road” huoneshwa katika kituo cha televisheni maarufu ya nchini China cha Hunan TV na hukadiriwa kutazamwa na watu zaidi ya milioni 220 kwenye TV huku kikifuatiliwa na watu takribani bilioni 3.07 kupitia mitandao mbalimbali ya kijamii ndani na nje ya China.

Aidha, kipindi hicho kimepata tuzo za kutajwa kuwa moja ya vipindi bora vya masuala ya safari (the top traveling show in China) na pia kutajwa kama alama ya vipindi vinavyoonesha uhalisia wa maisha (the new benchmark of reality shows).

Pamoja na wapigapicha na waandaaji wengine wanaofika 100 waliofika nchini kuandaa kipindi hicho, mastaa saba waliokuja kutoka tasnia za televisheni, filamu na muziki kwa ujumla wanawafikia watu zaidi ya milioni 500 kupitia mitandao yao mbalimbali ya kijamii akiwemo mwimbaji mashuhuri nchini humo Song Qian mwenye wafuasi milioni 46 kwenye mtandao wa kijamii wa Weibo pekee.

Kipindi cha Tanzania kinatarajiwa kurushwa Disemba mwaka huu wakati wa majira ya Sikukuu ya Krismas sambamba na vipindi vya nchi nyingine za Chile na Ufaransa.




Chapisha Maoni

0 Maoni