Rais Samia ahutubia SPIEF 2026, ahimiza ushirikiano na uwekezaji zaidi barani Afrika

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amehutubia Mkutano wa 29 wa Kimataifa wa Uchumi wa St. Petersburg (SPIEF 2026) nchini Urusi na kutoa wito wa kuimarishwa kwa ushirikiano wa kimataifa, uwekezaji na mahusiano ya kiuchumi na Afrika.

Akizungumza mbele ya wakuu wa nchi, viongozi wa serikali, wakuu wa makampuni na wawekezaji wa kimataifa, Rais Samia amesema dunia inapitia mabadiliko makubwa ya kiuchumi, kiteknolojia na kisiasa, hivyo kuna umuhimu wa kulinda mahusiano ya kibiashara na kujenga ushirikiano wenye kuleta ustawi wa pamoja.

Amesema Afrika ina nafasi kubwa katika ukuaji wa uchumi wa dunia kutokana na ongezeko la watu, kupanuka kwa masoko na kuimarika kwa ushirikiano wa kiuchumi kupitia Eneo Huru la Biashara la Bara la Afrika (AfCFTA).

Rais Samia ameeleza kuwa Tanzania inaendelea kujiimarisha kama lango muhimu la kuifikia Afrika kupitia uwekezaji katika miundombinu, usafirishaji, nishati, mageuzi ya kidijitali na viwanda.

Amesema uchumi wa Tanzania umeendelea kuimarika kutokana na ukuaji endelevu, utulivu wa kiuchumi na fursa ya kufikia soko la zaidi ya watu milioni 500 katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini.

Pia ametaja ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR), maboresho ya Bandari ya Dar es Salaam pamoja na maendeleo ya usafirishaji na muunganiko wa kidijitali kuwa sehemu ya uwekezaji unaobadili uchumi wa Tanzania.

Rais Samia amewaalika wawekezaji wa kimataifa kutumia fursa zilizopo katika sekta za madini, uongezaji thamani wa madini, kilimo, nishati, mafuta na gesi, viwanda, usafirishaji, utalii, dawa na teknolojia za kidijitali.

Amesema akiba kubwa ya madini adimu, rasilimali za gesi asilia na eneo la kijiografia la Tanzania vinaipa nchi nafasi ya kuwa kituo muhimu cha uwekezaji wa muda mrefu.

Kuhusu mahusiano ya Tanzania na Urusi, Rais Samia amesema nchi hizo zimeendelea kupanua ushirikiano katika biashara, uwekezaji, utalii, elimu na teknolojia, huku Tanzania ikiendelea kuimarisha uhusiano wa kiuchumi na Urusi pamoja na washirika wengine wa kimataifa.

Aidha, amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji na biashara ili kuchochea maendeleo endelevu na ajira, akieleza kuwa Tanzania iko wazi kwa biashara, uwekezaji, ubunifu na ushirikiano wa maendeleo jumuishi.



Chapisha Maoni

0 Maoni