Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amehutubia Mkutano wa 29 wa Kimataifa wa Uchumi wa St. Petersburg (SPIEF 2026) nchini Urusi na kutoa wito wa kuimarishwa kwa ushirikiano wa kimataifa, uwekezaji na mahusiano ya kiuchumi na Afrika.
Akizungumza mbele ya wakuu wa nchi, viongozi wa
serikali, wakuu wa makampuni na wawekezaji wa kimataifa, Rais Samia
amesema dunia inapitia mabadiliko makubwa ya kiuchumi, kiteknolojia
na kisiasa, hivyo kuna umuhimu wa kulinda mahusiano ya kibiashara na
kujenga ushirikiano wenye kuleta ustawi wa pamoja.
Amesema
Afrika ina nafasi kubwa katika ukuaji wa uchumi wa dunia kutokana na
ongezeko la watu, kupanuka kwa masoko na kuimarika kwa ushirikiano wa
kiuchumi kupitia Eneo Huru la Biashara la Bara la Afrika
(AfCFTA).
Rais Samia ameeleza kuwa Tanzania inaendelea
kujiimarisha kama lango muhimu la kuifikia Afrika kupitia uwekezaji
katika miundombinu, usafirishaji, nishati, mageuzi ya kidijitali na
viwanda.
Amesema uchumi wa Tanzania umeendelea kuimarika
kutokana na ukuaji endelevu, utulivu wa kiuchumi na fursa ya kufikia
soko la zaidi ya watu milioni 500 katika ukanda wa Afrika Mashariki
na Kusini.
Pia ametaja ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR),
maboresho ya Bandari ya Dar es Salaam pamoja na maendeleo ya
usafirishaji na muunganiko wa kidijitali kuwa sehemu ya uwekezaji
unaobadili uchumi wa Tanzania.
Rais Samia amewaalika
wawekezaji wa kimataifa kutumia fursa zilizopo katika sekta za
madini, uongezaji thamani wa madini, kilimo, nishati, mafuta na gesi,
viwanda, usafirishaji, utalii, dawa na teknolojia za
kidijitali.
Amesema akiba kubwa ya madini adimu, rasilimali za
gesi asilia na eneo la kijiografia la Tanzania vinaipa nchi nafasi ya
kuwa kituo muhimu cha uwekezaji wa muda mrefu.
Kuhusu
mahusiano ya Tanzania na Urusi, Rais Samia amesema nchi hizo
zimeendelea kupanua ushirikiano katika biashara, uwekezaji, utalii,
elimu na teknolojia, huku Tanzania ikiendelea kuimarisha uhusiano wa
kiuchumi na Urusi pamoja na washirika wengine wa kimataifa.
Aidha,
amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji
na biashara ili kuchochea maendeleo endelevu na ajira, akieleza kuwa
Tanzania iko wazi kwa biashara, uwekezaji, ubunifu na ushirikiano wa
maendeleo jumuishi.

0 Maoni