INEC yaalika vyombo vya habari kuomba vibali vya kuripoti Uchaguzi Mkuu 2025

 

Tume Huru ya Uchaguzi (INEC) imetoa mwaliko kwa vyombo vya habari vyenye nia ya kuripoti shughuli za kupiga kura, kuhesabu kura na kutangaza matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, kuwasilisha maombi ya kupata vibali rasmi.

Kupitia taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Uchaguzi, Kailima Ramadhani Kailima, tume hiyo imeeleza kuwa vyombo vyote vya habari vinavyotaka kushiriki katika kuripoti uchaguzi huo, vinapaswa kuwa na sifa mbili kuu kabla ya kuwasilisha maombi.

“Chombo cha habari kinapaswa kiwe kimesajiliwa kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari ya mwaka 2016, na pia kuhakikisha waandishi wake wamethibitishwa na Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, wakiwa na Press Cards halali zilizotolewa na bodi hiyo,” imeeleza sehemu ya taarifa hiyo.

INEC imefafanua kuwa maombi ya vibali hivyo yatawasilishwa kwa njia ya mtandao kupitia Mfumo wa Usajili wa Kibali ujulikanao kama Accreditation Management System (AMSA) unaopatikana kupitia kiungo: https://ams.inec.go.tz.

Dirisha la kupokea maombi litaanza rasmi Septemba 3, 2025 na kufungwa Oktoba 3, 2025.

Aidha, Mkurugenzi wa Uchaguzi Kailima amesisitiza kuwa Tume haitatoa rasilimali yoyote, iwe fedha au aina nyingine kwa vyombo vya habari vitakavyopata kibali, na kwamba vyombo hivyo vinapaswa kujitegemea kwa uendeshaji wa shughuli zao wakati wa uchaguzi.

Hatua hii inalenga kuhakikisha uchaguzi unafanyika kwa uwazi, huku vyombo vya habari vikichangia kwa weledi katika kutoa taarifa sahihi kwa umma kuhusiana na mchakato mzima wa uchaguzi.



Chapisha Maoni

0 Maoni