Daktari Bingwa wa Masuala ya Uzazi,
Dkt. David Mwesigye, amewataka wanaume kuacha tabia ya kuwalaumu au kuwaacha
wake zao pale wanaposhindwa kupata mtoto, akisisitiza kuwa tatizo la utasa
linaweza kumpata mwanamume au mwanamke.
Dkt. Mwesigye, ambaye ni mtaalamu wa
Kliniki ya Uzazi nchini Rwanda, alitoa ushauri huo wakati wa semina ya
waandishi wa habari kutoka nchi mbalimbali za Afrika, iliyoandaliwa na Taasisi
ya Merck Foundation kwa kushirikiana na Baraza la Habari Tanzania (MCT).
"Nawashauri wanaume wasikimbilie
kuwaacha wake zao wanaposhindwa kupata watoto. Wengine wamewaacha wake zao
wakidhani wao si tatizo, lakini baadaye wanashangaa kuona wake hao wamepata
watoto kwenye ndoa nyingine. Kumbe shida ilikuwa kwa mwanaume," alisema
Dkt. Mwesigye.
Alisema badala ya kufunga ndoa
nyingine, wanaume wanapaswa kutafuta ushauri wa kitaalamu kwani gharama za
vipimo na tiba ni nafuu ikilinganishwa na gharama za kuvunja ndoa na kuanzisha
nyingine.
Uelewa mdogo wa masuala ya uzazi wawakandamiza
wanawake
Dkt. Mwesigye alieleza kuwa kutokana
na uelewa mdogo wa masuala ya uzazi barani Afrika, wanawake wengi hujikuta
wakibebeshwa lawama za kukosa mtoto, mara nyingi wakihusishwa na utoaji wa
mimba wa zamani, ilhali sababu halisi zinaweza kuwa nyingi.
Sababu kuu za utasa
Miongoni mwa sababu alizozitaja kuwa
chanzo cha utasa ni pamoja na:
Lishe duni au uzito kupita kiasi.
Magonjwa ya zinaa yasiyotibiwa.
Maambukizi ya mfumo wa uzazi.
Upungufu wa kinga mwilini (kama virusi vya
UKIMWI).
Alitaja pia magonjwa ya zinaa
yanayosababisha utasa kwa wanawake kuwa ni Klamidia (Chlamydia) na Kisonono
(Gonorrhea), ambayo huathiri mfumo wa uzazi.
"Kwa Afrika, takriban asilimia 85
ya wanawake wanaopata huduma za utasa huwa wameathiriwa na maambukizi,
ikilinganishwa na asilimia 33 katika maeneo mengine ya dunia," alisema.
Bodaboda na matumizi ya kompyuta yapewa
tahadhari
Kwa upande mwingine, Dkt. Mwesigye
alionya kuwa wanaume wanaoendesha pikipiki kwa muda mrefu, maarufu kama
bodaboda, wako katika hatari ya kushuka kwa uzalishaji na ubora wa mbegu za
kiume kutokana na joto linalotokana na injini.
"Korodani hufanya kazi vizuri
katika joto la chini. Joto linalozalishwa na injini linaweza kuathiri
uzalishaji wa mbegu," alisema.
Aliwataka wanaume kuepuka kuoga maji
ya moto kwa kutumia hot tub, kutumia steam bath, kupakata kompyuta (laptop)
mapajani kwa muda mrefu, pamoja na mazingira yenye sumu za viwandani.
Lishe na mtindo wa maisha bora vinasaidia uzazi
Ili kuimarisha afya ya uzazi, Dkt.
Mwesigye alishauri kufanya mazoezi ya wastani, kula mlo kamili, kuepuka pombe,
sigara, dawa za kulevya na kupunguza vinywaji vyenye kafeini. Aliongeza kuwa
msongo wa mawazo ni moja ya sababu zinazochangia matatizo ya uzazi.
Ukeketaji na ndoa za utotoni vyatajwa kuchangia
utasa
Dkt. Francisca Bwalya kutoka Zambia
alizungumzia mila ya ukeketaji na ndoa za utotoni, ambazo bado zinaendelea
katika familia nyingi masikini barani Afrika, kuwa chanzo kingine cha utasa.
"Zaidi ya wanawake na wasichana
milioni 200 duniani wamekeketwa, hasa katika nchi za Kusini mwa Afrika na
mataifa ya Kiarabu. Ukeketaji husababisha maambukizi na matatizo ya mfumo wa
uzazi," alisema Dkt. Bwalya.
Aliongeza kuwa ndoa za utotoni
huwalazimisha wasichana kuingia kwenye majukumu ya uzazi kabla miili yao
haijakomaa, jambo ambalo huongeza hatari ya matatizo ya kiafya, ikiwemo utasa.
Jamii yatahadharishwa dhidi ya lugha za
unyanyapaa
Afisa Lishe kutoka Kenya, Bi.
Christine Nguku, alitoa wito kwa jamii kuacha kutumia lugha za unyanyapaa dhidi
ya wanawake wanaokosa watoto, kama vile:
“Lini utazaa?”, “Nizalie wajukuu
wangu”, “Hujui uchungu wa mwana kwa kuwa hujazaa”.
Alivitaka vyombo vya habari kuwa
mstari wa mbele katika kuelimisha jamii kwa mtazamo chanya na kumwonyesha
mwanamke anayepitia changamoto za utasa kama mtu jasiri, si mnyonge.
Mifano ya mataifa yanayotoa msaada wa tiba
Katika nchi kama Israeli, serikali
hutoa huduma za bure kwa wanandoa wenye changamoto ya utasa hadi watoto wawili.
Canada na Uingereza, kwa upande wao,
hutoa ruzuku ya serikali kwa watu wanaotafuta huduma za uzazi kwa njia ya
kitaalamu.
0 Maoni