Prof. Nagu asisitiza udhibiti wa magonjwa ya mlipuko

 

Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais – TAMISEMI (Afya), Profesa Tumaini Nagu, amewataka Maafisa Afya wa Mikoa na Halmashauri kote Tanzania Bara kuhakikisha wanachukua hatua madhubuti kupunguza magonjwa ya mlipuko, huku akiwasisitiza kuweka kipaumbele kwenye maeneo yenye changamoto ili yafanyiwe kazi kwa haraka.

Profesa Nagu alitoa kauli hiyo juzi jijini Mwanza wakati wa kufunga mkutano wa mwaka wa tathmini ya utekelezaji wa huduma za afya na usafi wa mazingira kwa mikoa na halmashauri zote, uliofanyika katika Ukumbi wa Rock City Mall kuanzia Julai 2 hadi Julai 5, 2025.

Akizungumza wakati wa kufunga mkutano huo, Profesa Nagu alisema ni muhimu kwa maafisa afya kutumia mkutano huo kwa kutoa taarifa sahihi na kwa wakati ili kusaidia katika kudhibiti magonjwa ya mlipuko ambayo yamekuwa tishio kwa afya ya umma.

“Ni muhimu sana kuwa na taarifa za wakati na sahihi kuhusu changamoto zinazojitokeza ili hatua zichukuliwe mapema. Hii ndiyo njia pekee ya kuzuia milipuko ya magonjwa isisambae zaidi,” alisema Prof. Nagu.

Mkutano huo ulilenga kutathmini hali ya utoaji huduma za afya na usafi wa mazingira, kubaini mafanikio yaliyopatikana, changamoto zilizopo na maeneo yanayohitaji ubunifu ili kuboresha huduma hizo kwa jamii.

Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Dkt. Jesca Lebba, aliwataka waganga wakuu wa mikoa kushiriki kikamilifu katika vikao kama hivyo kwa lengo la kuimarisha ushirikiano kati yao na maafisa afya.

“Tukiendelea kushirikiana kwa karibu kama wataalamu wa afya, tutafanikiwa kuondoa changamoto nyingi zinazokumba sekta hii, hasa kwenye afua za tiba na usafi wa mazingira,” alisema Dkt. Lebba.

Aidha, Mratibu Mkuu wa mkutano huo, Seleman Yondu, aliwakumbusha washiriki kuzingatia sheria, taratibu na miongozo ya kazi ili kuhakikisha matokeo chanya katika utekelezaji wa majukumu yao. Alisisitiza umuhimu wa ubunifu, bidii na weledi katika utendaji wa kila siku.

Kauli mbiu ya mkutano huo ilikuwa: “Utekelezaji wa afua za afya na usafi wa mazingira ni msingi wa kinga endelevu dhidi ya magonjwa na ustawi wa jamii.”

Mkutano huu wa siku nne umejikita katika kutoa fursa kwa maafisa afya kubadilishana uzoefu na kujifunza mbinu mpya zitakazosaidia kuimarisha huduma za afya nchini.



Chapisha Maoni

0 Maoni