REGROW yakabidhi magari sita mapya kwa TANAPA

Mradi wa Kuboresha  Usimamizi wa Maliasili na Kukuza Utalii Kusini mwa Tanzania (REGROW), leo tarehe 11, Novemba 2024 umekabidhi magari madogo sita (6) ya kwa ajili ya hifadhi za Nyerere, Ruaha, Mikumi na Udzungwa, Hifadhi ambazo ziko ndani ya mradi huo unaotekelezwa kusini mwa Tanzania.

Akipokea magari hayo Kamishna wa Uhifadhi TANAPA, Musa Nassoro Kuji aliishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuhakikisha kuwa uhifadhi unapata kipaumbele kupitia miradi mbalimbali kwa faida ya kizazi cha sasa na kizazi kijacho.

“Kupitia mradi huu, hadi sasa tumefanikiwa kupata jumla ya magari madogo 41 yakiwemo magari haya yanayokabidhiwa siku ya leo. Ninapenda kutoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa maono ya kuhakikisha kuwa uhifadhi unapata kipaumbele kupitia miradi mbalimbali na nitoe wito kwa hifadhi zinazofaidika na magari haya kuyatunza, na kuyatumia kwa malengo yaliyokusudiwa,”alisema Kamishna Kuji.

Aidha, Kamishna Kuji aliipongeza Benki ya Dunia kwa msaada wao katika kufanikisha mradi huu na kubainisha kuwa mchango wao si tu unasaidia juhudi za uhifadhi, bali pia unakuza uchumi wa jamii kupitia fursa za ajira na uwezeshaji wa jamii zinazozunguka hifadhi za Taifa.

Naye, Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi, Maureen Mwaimale ambaye ni mhasibu wa mradi wa REGROW alibainisha kuwa mradi huo umekabidhi magari madogo sita (6) ya nyongeza kwa ajili ya hifadhi za Nyerere, Ruaha, Mikumi na Udzungwa ikiwa ni ufadhili wa kupitia mkopo wa masharti nafuu uliotolewa na Benki ya Dunia kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuongeza kuwa magari hayo yana thamani ya jumla ya Shilingi za Kitanzania takribani milioni mia nane na ishirini na yatatumika kuongeza ufanisi katika ufuatiliaji wa athari za mazingira baada ya ukamilishwaji wa shughuli za ujenzi ndani ya hifadhi pamoja na kuwezesha jamii na kuhakikisha usalama wa jamii na mazingira (safe guard).

“Hifadhi zilizopo chini ya mradi wa REGROW zimekwishapokea vifaa vya doria, vifaa vya TEHAMA, mitambo ya barabara 16, malori makubwa 44 yakiwepo magari ya kutoa elimu ya uhifadhi (Cinema Vans and Epxedition Vehicles), matrekta saba, magari 41 yakiwemo haya sita,” alisema Kamishna Mwaimale.



 




Chapisha Maoni

0 Maoni