Kamishna Kuji asisitiza ushirikiano zaidi kufikia malengo ya TANAPA

 

Kamishna wa Uhifadhi TANAPA, Musa Nassoro Kuji amesisitiza ushirikiano ili kusukuma mbele jukumu la maendeleo ya Shirika na kutimiza malengo yaliyowekwa kwa wakati.

Kamishna Kuji, ameyasema hayo katika ziara yake aliyoifanya jana katika Hifadhi ya Taifa Tarangire ikiwa na lengo la kukagua utekelezaji wa shughuli za uhifadhi na utalii pamoja na kuzungumza na Maafisa na Askari uhifadhi waliopo katika hifadhi hiyo.

“Tushirikiane kwa pamoja ili kusukuma mbele jukumu la maendeleo ya Shirika letu na nisisitize kufanya kazi kwa pamoja kama timu moja ili tutimize malengo ya Shirika kwa wakati.”

“Tunapoona tunapata tuzo mbalimbali na kutambuliwa kimataifa ni kutokana na ushirikiano katika  kazi na mchango wa kila mmoja wetu, hivyo nasisitiza yule mkubwa kwa cheo na mdogo kuheshimiana na kuthaminiana ili kuleta tija katika utendaji kazi,” alisema Kamishna Kuji.

Aidha, Kamishna Kuji aliipongeza Hifadhi ya Taifa Tarangire kwa kuendeleza juhudi za kuhifadhi na kutangaza vivutio vilivyopo ili kuvutia wageni wengi zaidi kutembelea hifadhi hiyo ambayo ni hifadhi ya tatu kwa mapato katika Shirika.

Awali, akiwasilisha taarifa ya hifadhi, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi, Beatrice Kessy ambaye ni Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Tarangire alibainisha kuwa hifadhi hiyo kwa kipindi cha miezi minne ya mwaka huu wa fedha imeweza kukusanya kiasi cha shillingi Billioni 32 na kuongeza kuwa hifadhi hiyo imeandaa mkakati kabambe utakao kwenda kuvunja rekodi ya ukusanyaji wa mapato na kufikia kiasi cha shillingi billioni 100 ifikapo mwaka 2030.

Hifadhi ya Taifa Tarangire ni miongoni mwa hifadhi zilizopo katika Kanda ya Kaskazini na ni maarufu kwa makundi makubwa ya tembo wanaoonekana kwa urahisi na kuwa kivutio kikubwa kwa watalii wanaotembelea hifadhi hiyo.


     Na. Edmund Salaho/ Tarangire


Chapisha Maoni

0 Maoni