Mfanyabiashara na Mkazi wa Kata ya Ilangala, kisiwa cha
Gana, Nyamichere Ogunya Wilaya ya Ukerewe mkoani Mwanza amejitolea nyumba yake
aliyokuwa anaitumia na kuikabidhi kwa Jeshi la Polisi ili iwe Kituo cha Polisi
kwa ajili ya kutoa huduma za Usalama kwa wakazi zaidi ya 6,000 wa kisiwa hicho.
Nyumba hiyo yenye vyumba zaidi ya 15 imekabidhiwa kwa
Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoa wa Mwanza (SACP) Wilbroad Mutafungwa ambapo
amemshukuru mfanyabiashara huyo, na kusema baada ya nyumba hiyo kufanyiwa
marekebisho kwa kuwekewa miundombinu na mifumo ya majitaka itakayokidhi hadhi
ya Kituo cha Polisi itaanza kutumika kutoa huduma kwa wakazi wa kisiwa hicho.
"Nimpongeze mfanyabiashara aliyejitolea nyumba yake
kuwa kituo cha polisi na ikiwezekana marekebisho ya kituo hiki natamani yaishe
mwishoni mwaka mwaka huu ili mwezi Januari 2024 pengine kituo hicho kiwe
kimekamilika na mimi nitatamani sana kuja kukizindua hiki kituo ili tuweke
askari wa kutosha kuanza kufanya kazi," amesema Kamanda Mutafungwa.
Swai Somba ni mvuvi wa kisiwa hicho ameliomba Jeshi la
Polisi kusaidia kukamilisha mapema marekebisho ya kituo hicho ili huduma ianze
kutolewa itakayosaidia kukomesha vitendo vya uhalifu huku akiomba mipaka
inayotenganisha Tanzania na Uganda iwekwe ziwani ili kupunguza matukio ya
wavuvi wa pande hizo mbili kuingiliana.
"Sisi wavuvi wadogo tunapotoka hapa kisiwani kuingia ziwani
huko kuvua huwa tunanyanyasika sana kutokana na vyombo vyetu mfano sisi wavuvi
wa kasia huwa uvuvi wetu ni duni lakini wanaotumia mashine wametuwekea masharti
ambayo mimi ninashindwa kujua moja wapo ukitoka ziwani ukileta hapa samaki
unaanza kuulizwa umetumia zana gani kuvua wakati huenda ulikuwa na ndoano,
tunaomba msaada katika hili," amesema Somba.
Mwenyekiti wa Kamati ya ushauri na uvuvi endelevu Ziwa
Victoria, Bakari Kadabi amesema, kuanzia Januari 2024, Serikali inatarajia
kuweka mipaka ziwani itakayokuwa inawasaidia wavuvi kujua upande wa Tanzania na
Uganda.
"Kuhusu mipaka Serikali imejipanga kuanzia mwezi
Januari kuweka maboya mpakani kati ya Tanzania na nchi jirani kwa hiyo tatizo
la kuingilia linaenda kuisha kabisa ila niwaombe wavuvi muwe wakweli hamna
sababu ya kwenda kuvua upande wa Uganda wakati huku tuna maeneo mengi ya
kuvua," amesisitiza Kadabi.
Katika hatua nyingine, Kamanda Mutafungwa ametangaza kufanya oparesheni kabambe na endelevu ndani ya Ziwa Victoria na maeneo mengine ili kutokomeza uhalifu na kuimarisha ulinzi na usalama zaidi katika maeneo yote.
0 Maoni